Banner KICHWA CHAKO KINA NYWELE NA UBONGO PIA | Darasa La Maisha - Maisha Mafanikio

0

“Upo sehemu ulipo leo sababu mawazo yako yamekufikisha hapo ulipo. Kesho utakuwa pale mawazo yako yatakapo kufisha.”James Allen.

Ulimwengu wako wa nje unatawaliwa na ulimwengu wa ndani yaani mawazo yako. Ubora wa ufahamu wako au fikira zako ndiyo unatangaza hatima ya maisha yako ya kesho. Kama mawazo ndiyo yanaongoza maisha yako basi kuwa na ufahamu wenye nguvu ni muhimu sana. Kuwa na ufahamu legevu ni hatari sana kuliko hata ulegevu wa viungo vya mwili.

 Kuna watu wengi ambao wana ulemavu wa viungo vya mwili lakini kwa sababu ufahamu wao ni imara, hauna ulemavu, wanaishi maisha ya furaha na ya mafanikio. Kwa upande mwingine kuna mamilioni ya watanzania na walimwengu ambao wanaishi maisha yasiyo na msimamo licha ya kwamba hawana ulemavu wowote, hii ni kwa sababu wana ulegevu wa ufahamu. 

Nguvu ya mawazo yako ni nishati muhimu sana katika kukuwezesha kuyatimiza maono uliyonayo, yaani ili vitu na mipango uliyonayo ndani ya ufahamu wako viwe halisi katika ulimwengu wa nje lazima uwe na ufahamu wenye nguvu. Kuyabadilisha mawazo yako ili yawe kitu halisi lazima uwe na ufahamu imara.

Ufahamu wenye nguvu  ni kani  ya mabadiliko yoyote unayotaka kuyapata katika maisha yako. Ukiwa mlegevu katika kuwaza na katika kuyawekea msimamo yale unayoyawaza daima utakuwa mtu yule yule. Maisha yako yatakuwa juzi kama jana na jana kama leo. Hautapiga hatua za mafanikio ya kiuchumi wala kitabia kadhalika kimwonekano.

Ufahamu imara ni ule wenye mazoea ya kujipa muda kutafakari kwa kina kila jambo unalotaka kulitekeleza. Kabla ya kufanya jambo ujizoeshe kulitafakari kwa kina. Ufahamu kwa nini unalitenda, manufaa yake na athari zake, changamoto zake pia ufahamu uhalali wa hilo jambo kiimani yako ya dini, kitamaduni na kimazingira uliyopo.

Mtu mwenye ufahamu imara hatakiwi kufanya vitu kwa kukurupuka au kwa kufuata hisia tu. Kwa bahati mbaya sana matokeo ya watu wengi kushindwa kutimiza mambo waliojipangia ni kujiingiza kwenye hayo masuala kichwa kichwa bila kuhoji na kujihoji. Mambo mengi sana yanayowaumiza watu leo ni matokeo ya kufanya mambo bila tafakari ya kina.

 
Fikiri mtu anaanza mahusiano wa kimapenzi ghafla tu kwenye chombo cha usafiri au kwenye mitandao au mtu anaanza mahusiano ya kimapenzi kutokana na kuvutwa na kazi au cheo cha mwenzie, na wakati mwingine mtu anaingia kwenye mahusiano kwa kuvutwa na mavazi maradadi ya mtu pekee.

 Mipasuko mingi ya mioyo ya watu kutokana na kuachwa, kuachana, kuachwa  au usaliti ni matokeo ya kutokufikiri vema kabla ya kuamua. Mimba nyingi zinazotolewa leo ni matokeo ya kuingia kwichwa kichwa kwenye mapenzi na ngono hivyo hata inapotokea mimba kuna kosekana utayari wa kulea.

Ufahamu imara ufanya maamuzi baada ya sala binafsi, utafiti binafsi na kushauriwa na watu wenye hekima. Sehemu kubwa ya watu siku hizi hawalipi uzito suala la sala na dua kabla ya kufanya maamuzi yaliyo mbele yao. Wengi hufikiri sala haina cha kufanya na maamuzi wanayochukua jambo ambalo ni kosa kuu.

 Ikiwa unaamini uliumbwa na Mungu naye ni mkuu wa yote basi mshirikishe katika kila jambo. Sala ina nguvu ya kuimarisha ufahamu kwa sababu inakufunulia vitu ambavyo huwezi kuviona kwa macho ya kawaida, inakupa maonjo ya matumaini kadhalika inakuondolea woga.

Maisha ni mchezo wa tahadhari sana ambao hakuna anayeweza kushinda bila kutumia uzoefu fikra angavu, elimu ,vipaji na na ushauri wa watu wengine. Kutafuta ushauri kwa watu wenye hekima na uelewa juu ya jambo unalotaka kufanya ni muhimu sana.

 Kumbuka si kila mtu anaweza kukushauri sahihi, si kila ndugu, mzazi, kiongozi au rafiki anaweza kukushauri sahihi. Ili kujiimarisha kiufahamu jifunze kutaka ushauri kwa wenye hekima .

Kuhusu kutaka ushauri kwa watu pia ipo kasoro kwa baadhi ya watu, wao hutaka ushauri juu ya jambo fulani kabla ya kujishauri. Wao ushauri wanaopewa na watu wa nje wanauamini zaidi kuliko ushauri wanaojishauri. Ni muhimu kujishauri wewe kabla ya kushauriwa, hata baada ya kushauriwa inakupasa kupembua huo ushauri uliopewa, si kila unaloshauriwa ni sahihi.

Fahamu kuwa hakuna anayekufahamu wewe zaidi ya unavyojifahamu wewe mwenyewe. Wewe unafahamu zaidi nini unapendelea na nini haupendi, moyo wako ni mshauri wako wa kwanza ukiupa nafasi.

 Usiruhusu watu wa nje watawale maisha yako kwa kiasi kikubwa, maisha yako yanakuhusu zaidi wewe, usiamuliwe kila kitu cha kufanya, namna ya kufanya na wakati wa kufanya. Uko tofauti. Tafuta ushauri, sikiliza ushauri lakini kumbuka kuna wakati wa kufanya maamuzi wewe pekee. Ukiwa msikiliza ushauri na mtekelezaji bila kujihoji mara mbilimbili maisha yako hayatakuwa na msimamo.

Yako mambo mengine katika maisha yako yanahitaji maamuzi ya haraka na magumu. Haya hauhitaji kutafuta ushauri. Masuala mengine unayotaka kufanya watu hawawezi kukuelewa hata ukitumia miezi saba kufafanua ili wa kuelewe hawatakuelewa, haya yanahitaji hekima yako kuyafanya.

Sio kila utakachotaka kukifanya katika maisha yako watu wa karibu yako watakuelewa, yako ambayo hayaeleweki mwanzoni lakini yanaeleweka mwishoni baada ya kwisha kutendeka. Hivyo usichelewe kufanya maamuzi kwa sababu unasubiri watu wote wakuelewe na wakupe kibali.

Masuala ambayo ndani yako unayapa uzito sana lakini wengine wanaona ni ya kawaida, ukingojea siku wakuelewe utabaki kama ulivyo siku sote. Unatakiwa kujizoesha kuiamini akili yako, kichwa chako kina  nywele na ubongo pia.

Chemchemi3.blogspot.com/  #Darasa la Maisha

 

 

 

 

Post a Comment

 
Top